Katika wiki za hivi karibuni, picha za mifugo iliyodhoofika katika eneo linalokabiliwa na ukame karibu na mpaka wa Somalia zimewashtua wengi katika eneo ambalo tayari limeathirika kutokana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa.
Katika miaka ya hivi karibuni, msimu wa mvua umefupishwa kwa baadhi ya jamii, na kuwafanya wawe katika hatari zaidi ya ukame. Kwa kawaida, wanyama ndio wa kwanza kufa.
Hasara hizi za mifugo zinakumbusha hali iliyotokea kati ya mwaka 2020 na 2023, kipindi ambacho mamilioni ya wanyama walikufa katika eneo hilo kuanzia Kenya hadi sehemu za Ethiopia na Somalia. Wakati huo, njaa iliyotabiriwa nchini Somalia iliepukwa kutokana na ongezeko kubwa la misaada ya kimataifa.
Misimu minne mfululizo ya mvua imekuwa na upungufu katika sehemu za Pembe ya Afrika, ambayo huelekea Bahari ya Hindi.
Msimu wa mvua, kuanzia mwezi Oktoba hadi mwezi Desemba, ulikuwa mmoja wapo wa msimu mkavu zaidi kuwahi kurekodiwa, kulingana na Shirika la Afya Duniani (WHO). Kutokana na mvua iliyonyesha kwa kipindi kifupi, baadhi ya maeneo ya mashariki mwa Kenya yalikumbwa na ukame mkali zaidi wa msimu tangu mwaka 1981.
Takriban kaunti kumi nchini Kenya zimeathiriwa na ukame, kulingana na Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Maeneo ya Ukame (NDMA).
Kaunti ya Mander, kaskazini mashariki mwa nchi, inayopakana na Somalia, imefikia kiwango cha juu cha tahadhari, ikimaanisha kuwa uhaba mkubwa wa maji umesababisha vifo vya mifugo na udumavu miongoni mwa watoto.
Mwishoni mwa mwezi Januari, WHO iliripoti kwamba mateso hayo yanaenea hadi Somalia, Tanzania, na hata Uganda, ambapo idadi kubwa ya watu wanatishiwa na hali kama hiyo ya hewa na uhaba wa maji.
Kusini mwa Somalia, tathmini ya shirika la kibinadamu la Islamic Relief imefichua uhaba wa chakula unaotisha huku familia zikikimbia ukame unaozidi kuwa mbaya katika eneo hilo.
Nchini Somalia, nchi ambayo kwa muda mrefu imekuwa katika hatari ya ukame, zaidi ya watu milioni 3 wamehama makazi yao na kutafuta hifadhi katika kambi za wakimbizi wa ndani.
Lakini msaada unaotolewa hautoshi. Huko Baidoa, 70% ya watu waliokimbia makazi yao wanaishi kwa mlo mmoja tu kwa siku, Islamic Relief imesema katika taarifa. Shirika hilo liliongeza kuwa watoto katika kambi "wanaonyesha dalili zinazoonekana za utapiamlo na unyonge."
Kulingana na wataalamu, matukio mengi haya yanatokana na mabadiliko ya hali ya hewa.
Bahari ya Hindi imeongezeka joto, na kusababisha baadhi ya dhoruba kali zaidi za kitropiki katika miaka ya hivi karibuni. Wakati huo huo, ukame umekuwa mkali zaidi na umechukuwa kipindi kirefu.
Yote haya ni mabaya kwa Waafrika, ambao uchumi wao unategemea sana kilimo kinachotegemea na mvua, na kuwafanya wawe katika hatari ya matukio mabaya ya hali ya hewa. Wakulima wengi wanasema kwamba kuongezeka kwa hali ya joto kunawanyima mifugo yao ardhi ya malisho na kuharibu mazao yao.
Afrika iko katika hatari kubwa ya matukio mabaya ya hali ya hewa kwa sababu haina vifaa vya kutosha kujiandaa kwa majanga ya asili. Ingawa inachangia asilimia 3 hadi 4 tu ya uzalishaji wa hewa chafu duniani, kulingana na Umoja wa Mataifa, bara hilo ni mojawapo ya yaliyo katika hatari zaidi ya athari za mabadiliko ya Tabianchi.