MAFUTA YASHUKA BAADA YA USITISHWAJI WA MAPIGANO

Bei ya mafuta katika masoko ya kimataifa imeshuka kwa kiasi kikubwa kufuatia tangazo la Rais wa Marekani, Donald Trump, la kufikiwa kwa makubaliano ya kusitisha mapigano kwa muda wa wiki mbili, hatua iliyorejesha matumaini ya utulivu wa hali ya kisiasa na kiuchumi duniani.

Kabla ya tangazo hilo, pipa la mafuta lilikuwa likiuzwa kwa wastani wa dola 103.42 (Tsh 305,089), ikiwa ni punguzo kutoka viwango vya juu vilivyoshuhudiwa mwanzoni mwa mzozo, ingawa bado bei hiyo iko juu ikilinganishwa na kipindi cha kabla ya mvutano huo kuanza mwishoni mwa Februari.

Mtaalamu wa uchumi wa nishati kutoka Japan, Ichiro Kutani, ameeleza kuwa kushuka kwa bei kunatokana moja kwa moja na matarajio ya kurejea kwa amani, huku akionya kuwa bei haitarejea haraka katika kiwango cha kawaida cha dola 70 kwa pipa kutokana na uharibifu mkubwa wa miundombinu ya nishati katika baadhi ya maeneo ya Mashariki ya Kati.

Wakati huo huo, masoko ya hisa barani Asia yameonyesha kuimarika, ambapo Nikkei 225 imepanda kwa takribani asilimia 4 na ASX 200 kwa asilimia 3, ishara ya kurejea kwa imani ya wawekezaji duniani.

Hata hivyo mabadiliko hayo yanaashiria kupungua kwa hofu ya kuyumba kwa uchumi wa dunia, huku sekta ya nishati na biashara za kimataifa zikitarajiwa kupata nafuu endapo hali ya amani itaendelea kudumu.

10YrsJembefm  #Familiamoja #AhsantekwaTime

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii