Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Kenani Laban Kihongosi leo Agosti Mosi mwaka huu mekutana na kuzungumza na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania Mhe. Marianne Louise Young, wakikubaliana Uongozi wa Mkoa wa Arusha na Uingereza kuendelea kushirikiana katika kukuza na kuimarisha sekta ya afya na Utalii Mkoani Arusha.
Balozi Young yupo Mkoani Arusha akiambatana na Mkuu wa Diplomasia ya uchumi wa Ubalozi wa Uingereza nchini Bi. Tammy Clayton, wakitembelea na kukagua miradi mbalimbali inayofadhiliwa na Serikali ya Uingereza, akikutana pia na kuzungumza na Wafanyabiashara na Wawekezaji kutoka nchini Uingereza waliowekeza kwenye sekta ya Utalii Kanda ya Kaskazini na walio na makao makuu yao Mkoani Arusha.
Katika mazungumzo yao, Mhe. Kihongosi amemuhakikishia Balozi Young kuwa Mkoa wa Arusha ni salama na tulivu kwa kila Mgeni na Mtalii anayefika Mkoani hapa, akibainisha kuwa Ofisi yake ipo wazi kwa wenyeji, wageni na Watalii wenye ushauri na wenye kukutana na changamoto wawapo Mkoani hapa kwa shughuli mbalimbali ili Ofisi yake iweze kushughulikia changamoto zinazojitokeza.
"Tumedhamiria kuimarisha shughuli za Utalii Mkoani Arusha sambamba na kuwawezesha Wananchi wanaojishughulisha na Utalii kama sehemu ya kukuza uchumi na ustawi wa wananchi na Taifa kwa Ujumla. Tunaimarisha pia miundombinu ya usafiri ili kuvutia watalii zaidi ambapo kupitia Programu ya TACTIC, kuanzia mwezi huu serikali inajenga barabara zaidi ya Km. 30 hapa Mjini na zile za ndani ya hifadhi ya Ngorongoro ili ziweze kupitika misimu yote ya mwaka." Ameeleza Mhe. Kihongosi.
Akijibu kuhusu Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29 mwaka huu Mkuu wa Mkoa wa Arusha amemuhakikishia Balozi Young utulivu na usalama katika kipindi chote cha uchaguzi Mkuu mkoani Arusha, akibainisha kuwa Uchaguzi huo hautoathiri shughuli za utalii, akitoa pia ukaribisho kwa Raia wa kigeni na wenyeji kuendelea kutembelea vivutio vya utalii vinavyopatikana Mkoani Arusha.
Kadhalika katika maelezo yake Balozi Young pia amekaribisha maeneo mapya ya uwekezaji na yenye kuhitaji msaada wa Serikali ya Uingereza Mkoani Arusha, akiahidi kushirikiana na Uongozi wa Mkoa wa Arusha chini ya Mhe. Kihongosi katika kuhakikisha huduma za Kijamii na kiuchumi zinaimarika zaidi kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha.
Kulingana na Balozi Young, takribani Raia wa kigeni 80, 000 kutoka nchini Uingereza waliitembelea Tanzania mwaka 2024, wengi wao wakifika kutalii Mkoani Arusha na Zanzibar, akibainisha kurejea Arusha pia mwanzoni mwa Wiki Ijayo yeye na familia yake ili kusherehekea siku yake ya kuzaliwa ndani ya hifadhi ya Ngorongoro Mkoani hapa.