Raila Odinga Junior "Baba Atakuwa Ikulu Asubuhi na Mapema".

Raila Odinga Junior, kitinda mimba wa kinara wa ODM Raila Odinga, amebashiri ushindi mkubwa wa muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Kupitia kwa mtandao wa Twitter, Junior alisema kuwa babake atambwaga asubuhi mpinzani wake wa karibu Naibu Rais William Ruto ambaye anapeperusha bendera ya muungano wa Kenya Kwanza.


Junior vilevile alisifia uteuzi wa kiongozi wa chama cha Narc Kenya Martha Karua kuwa mgombea mwenza wa Raila, akitaja uteuzi huo kama chaguo bora alilofanya babake.
“Ifikapo saa mbili asubuhi, Baba atakuwa Ikulu. Chaguo bora la naibu wa rais wa kwanza mwanamke,” Junior alisema.
Katika hafla iliyoandaliwa katika ukumbi wa KICC mnamo Jumatatu, Mei 16, Raila alimtaja Martha Karua kuwa mgombea mwenza wa muungano wa Azimio-OKA katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Karua aliibuka mshindi kwa nafasi hiyo mbele ya kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, magavana Charity Ngilu (Kitui), Hassan Joho (Mombasa), Lee Kinyanjui (Nakuru) na Wycliffe Oparanya (Kakamega), Mwakilishi wa Kike wa Murang'a Sabina Chege, Waziri wa Kilimo Peter Munya na aliyekuwa Mbunge wa Emgwen Stephen Tarus.
Kabla ya kutangazwa kwa jina hilo, viongozi wanawake wanaoegemea upande wa Raila pia walikuwa wamemwidhinisha Karua kuwa mgombea mwenza katika Azimio.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii