TMA yatoa tahadhari ya mvua kubwa kuanzia kesho

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari ya siku tatu kuhusu uwezekano wa mvua kubwa zitakazoweza kusababisha mafuriko katika baadhi ya mikoa ya ukanda wa Pwani, ikiwemo Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo  Aprili 7, 2026, mvua hizo zinatarajiwa kuanza kesho Jumatano hadi Ijumaa, zikihusisha mikoa ya Lindi, Mtwara, Tanga na Pwani pamoja na Jiji la Dar es Salaam, sambamba na visiwa vya Unguja na Pemba.

AidhaTMA imeeleza kuwa uwezekano wa mvua hizo pamoja na athari zake uko katika kiwango cha kati, huku wananchi wakitakiwa kuchukua tahadhari zote muhimu ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza.

“Kuanzia kesho hadi Ijumaa, mvua zinatarajiwa kunyesha katika maeneo tajwa. Uwezekano na athari zake zipo katika kiwango cha kati,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

Hata hivyo, mamlaka hiyo imeonya kuwa mvua hizo zinaweza kusababisha mafuriko katika baadhi ya maeneo na kuathiri shughuli za kijamii na kiuchumi, hivyo wananchi wanashauriwa kufuatilia taarifa za hali ya hewa na kuchukua hatua za kujikinga.

10YrsJembefm  #Familiamoja #AhsantekwaTime

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii