Waziri mkuu wa zamani wa Burundi, Jenerali Alain-Guillaume Bunyoni, ambaye anatumikia kifungo cha maisha gerezani kwa jaribio la mapinduzi, hapo jana aliachiwa kwa sababu za kiafya.
Bunyoni ambaye wakati mmoja alikuwa mwanasiasa mwenye nguvu kwenye taifa hilo, alihudumu kama Waziri Mkuu kuanzia mwaka 2020 hadi 2022, wakati alipofutwa kazi siku chache kupita tangu rais Evariste Ndayishimiye atoe madai kwamba kulikuwa na jaribio la mapinduzi.
Mashirika ya haki za binadamu yamedai kuwa hali ya kiafya ya mwanasiasa huyo anaeysumbuliwa na ugonjwa wa kisukari ilizidi kuwa mbaya gerezani kutokana na kukosa dawa na pia alianza kupooza na kushindwa kuongea.
Bunyoni amekuwa hospitalini tangu mwezi Oktoba mwaka jana akipatiwa matibabu, lakini akaachiwa huru kwa masharti ya kitabibu, vyanzo hivyo vimesema.
Bunyoni ambaye aliwahi kuwa mkuu wa polisi na Waziri wa mambo ya ndani ya nchi, alionekana kuwa na ushawishi mkubwa katika jeshi na hasa kwa maofisa wa juu waliokuwa wanashawishi siasa za Burundi hadi alipokamatwa mwezi April mwaka 2023.