Yanga ilianzishwa mwaka 1935 na Simba mwaka
1936, lakini ukizama ndani utagundua kwamba , huo ndiyo ulikuwa mwanzo
wa utani na upinzani wa jadi baina ya miamba hiyo ya soka nchini.
Kulikuwa kuna timu inaitwa New Youngs ambayo mwaka 1938 ilisambaratika
na baadhi ya wachezaji wake wakaenda kuunda timu iliyokuwa Sunderland,
ambayo hivi sasa inajulikana kama Simba.
Kabla ya kutokea vurugu zilizoisambaratisha New Youngs vijana wa Dar es
Salaam walikuwa na desturi ya kukutana viwanja wa jangwani kufanya
mazoezi na baada ya muda wakaamua kuunda timu yao, waliyoipachika jina
Jangwani Boys.
Ndani ya kipindi kifupi timu hiyo iliteka hisia za wengi, waliojitokeza
kujiandikisha uanachama wa klabu hiyo, miongoni mwao waliovutiwa na
uanachama wa klabu hiyo ni Tabu Mangala (Sasa marehemu) na ilipofika
mwaka 1926 walifanya mkutano wa kwanza katika eneo ambalo hivi sasa kuna
shule ya sekondari ya Tambaza.
Miongoni mwa yaliyojadiliwa kwenye mkutano huo ni kuiboresha timu hiyo
ambayo wachezaji wake wengi walikuwa wafanyakazi wa bandarini na
mashabiki wake wengi walikuwa wabeba mizigo bandarini.
Baada ya mkutano huo, timu ilibadilishwa jina na kuwa Navigation,
iliyotokea kuwa moto wa kuotea mbali katika timu za waafrika enzi hizo,
kabla ya uhuru wa Tanganyika.
Timu kama Kisutu, Kitumbini, Gerezani na Mtendeni zilikuwa hazifui dafu kwa wana wa Jangwani hao.