VIONGOZI wa Kiislamu wameonya kwamba huenda jamii yao itajitenga na mfumo wa kisheria wa Kenya iwapo serikali haitachukua hatua ya kufuta au kurekebisha hukumu ya Mahakama ya Juu kuhusu haki ya watoto waliozaliwa nje ya ndoa kurithi mali.
Wakizungumza mjini Mombasa, wakiongozwa na Sheikh Abu Katada, walitaja hukumu hiyo kuwa “kisingizio cha kuvunja misingi ya sheria ya Kiislamu” na kudhalilisha mamlaka ya afisi ya Kadhi Mkuu.
“Hii ni njama fiche ya kuidhoofisha afisi ya Kadhi Mkuu. Sheria ya Kiislamu imeweka wazi masuala ya urithi. Mambo haya hayawezi kuamuliwa na mahakama ya kidunia.
Ikiwa serikali itazidi kupuuza misimamo ya dini yetu, basi tutalazimika kuanzisha utawala wetu wa Kiislamu,” Bw Athman Shariff alionya.
Kulingana na viongozi hao, Katiba ya Kenya imeipa afisi ya Kadhi Mkuu mamlaka ya kuamua masuala ya ndoa, talaka na urithi kwa mujibu wa sheria ya Kiislamu, lakini hukumu hiyo ya Mahakama ya Juu ni kinyume na hayo.