Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, imewahukumu kunyongwa hadi kufa maofisa wawili wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara, waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya mauaji ya mfanyabiashara wa madini, Mussa Hamisi (25), mkazi wa Kijiji cha Ruponda, Wilaya ya Nachingwea, Mkoa wa Lindi.
Hukumu hiyo imetolewa leo Jumatatu, Juni 23, 2025 na Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara chini ya Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Hamidu Mwanga.
Maofisa waliokutwa na hatia ni Mrakibu wa Polisi, Gilbert Kalanje, aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Mtwara na Mrakibu Msaidizi wa Polisi, Charles Onyango, aliyekuwa Mkuu wa Kituo cha Polisi Mtwara.