FIFA kuichunguza Argentina juu ya madai ya ubaguzi

Shirikisho la soka duniani FIFA linachunguza video inayoonyesha wachezaji wa timu ya taifa ya Argentina wakiimba nyimbo kuhusu wachezaji wa Ufaransa zilizotafsiriwa na shirikisho la soka la Ufaransa kuwa za "kibaguzi.”

Shirikisho la soka la Ufaransa FFF limesema kuwa litawasilisha malalamiko kwa FIFA kuhusu video hiyo, ambapo wachezaji wa Argentina walikuwa wanaimba juu ya asili ya Kiafrika ya mshambuliaji Kylian Mbappe.

Video hiyo ilichapishwa na kiungo Enzo Fernandez katika ukurasa wake wa Instagram wakati timu hiyo ilipokuwa inasherehekea ushindi wake dhidi ya Colombia katika fainali ya Kombe la Copa America.

Fernandez anayechezea klabu ya Chelsea baadaye aliomba msamaha kwenye mtandao wake wa kijamii.

Makamu wa rais wa Argentina Victoria Villarruel amemtetea Fernandez na timu ya taifa ya Argentina japo ameeleza kuwa hawezi kuvumilia vitendo vya "nchi ya kikoloni.”


Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii