• Ijumaa , Mei 9 , 2025

Ally Kamwe "Hatuna tatizo na Al Merreikh"

Kikosi cha Young Africans kinatarajia kuondoka nchini leo Alhamis (Septemba 14) kuelekea Rwanda kwa ajili ya kuwafuata Al Merrikh kutoka Sudan katika mechi ya kwanza ya hatua ya kwanza ya mashindano ya kimataifa ya Ligi ya Mabingwa Afrika itakayochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Pele Kigali.

Mechi ya marudiano ya timu hizo itachezwa Septemba 29, mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es salaam na mshindi wa jumla atatinga hatua ya makundi ya michuano hiyo inayosimamiwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).

Afisa Habari wa Young Africans, Ali Kamwe, alisema anaamini mechi hiyo itakuwa ngumu kwa sababu timu wanayocheza nayo ni kubwa na ina uzoefu katika michuano hiyo.

Kamwe alisema pia kila upande umejiandaa vyema kusaka matokeo chanya katika mechi ya kwanza na kujiweka kwenye mazingira bora kuelekea mchezo wa marudiano.

Alisema wachezaji wao wamejipanga kucheza katika kiwango bora katika dakika 90 za mechi ya kwanza kwa sababu wanataka kufikia malengo.

“Hatuna tatizo na Al Merrikh, tunatambua ni klabu kubwa, kongwe na huwa inafanya vizuri kwenye hii michuano, ila msimu huu inatakiwa wajipange vizuri kama sisi tulivyojipanga, dakika 90 za pale Kigali ndizo zitatupa nini kitakuja kutokea katika mechi ya marudiano jijini Dar es salaam, tunajua utakuwa mchezo mgumu sana lakini tuna imani kubwa na benchi letu la ufundi, tuna imani kubwa na wachezaji wetu.

“Pia tuna imani kubwa ya hamasa ya wanachama na mashabiki wetu ambao watasafiri kutoka Dar kwenda nchini Rwanda kwa ajili ya mechi hiyo kwa sasa hesabu ya haraka haraka ni jumla ya wachezaji 36 wamejaa, lakini kuna mashabiki ambao wapo maeneo ya mipakani ambao wanasema watasafiri asubuhi siku ya mechi na kurejea baada ya kumalizika,” alisema Kamwe.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii