Tshisekedi na Fayulu kupambana tena katika uchaguzi wa rais wa DRC hapo Disemba 20, 2023

Tshisekedi anagombania mhula wa pili katika taifa lenye utajiri mkuu wa cobalt duniani, baada ya kushinda katika mhula wa kwanza ulokuwa na utata mwaka 2018.

Wajumbe wa mungano wa Union Sacree unaohusisha wanasiasa maarufu wa Kongo kama waziri wa ulinzi Jean Pierre Bemba na waziri wa uchumi Vital Kamerhe, walimchagua Tshisekedi kwa sauti mmoja.

Utawala wake umekumbwa na hali ngumu ya uchumi, janga la Covid 19, mlipuko wa Ebola, ukosefu wa usalama hasa mashariki ya nchi ambako wapiganaji wa kundi la M23 waliteka sehemu ya maeneo ya mashariki na kusababisha kuvunjika kwa uhusiano na Rwanda.

Tshisekedi, kijana wa mwanasiasa mashuhuri wa upinzani Etienne Tsisekedi, aliyeahidi kupambana na ulaji rushwa na utawala wa kimabavu anakanusha tuhuma kutoka makundi ya kutetea haki za binadama na wakosowaji wake, kwamba ameshindwa kutekeleza ahadi zake.

Mmoja kati ya mpinzani wake mkuu, kiongozi wa upinzani Martin Fayulu aliyeshindwa na Tshisekedi mwaka 2018, alithibitisha Jumamosi, Septemba 30, 2023 kwamba atagombania tena kiti cha rais baada ya awali kutishia kwamba ataususia uchaguzi ili kulalamika dhidi ya ubaridhirifu unaotokea katika kuandikishwa kwa wapiga kura.


Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii