Msajili Aikalia Kooni TLP Nafasi ya Mrema Wapewa Agizo Kufanya Uchaguzi

OFISI ya Msajili wa Vyama vya Siasa, imekitaka Chama cha Tanzania Labpour Party (TLP), kuitisha uchaguzi wa kujaza nafasi ya mwenyekiti wake taifa, iliyoachwa wazi na Augustino Mrema, aliyefariki dunia Agosti 2022.

Agizo hilo limetolewa na ofisi hiyo kupitia barua yake iliyotolewa na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Sisty Nyahoza, mwishoni mwa Juni mwaka huu, akijibu malalamiko ya baadhi ya wanachama wa TLP kuhusu kusitishwa kwa uchaguzi wa chama hicho zaidi ya mara mbili pasina sababu za msingi.

“Ibara ya 24 ya katiba ya TLP inaeleza kuwa, nafasi ya uongozi ikiwa wazi inapaswa kujazwa mara moja. Hivyo kwa kuwa Mrema alifariki tarehe 21 Agosti 2022 na TLP mlipanga kufanya uchaguzi kujaza nafasi hiyo tarehe 6 Machi 2023 uchaguzi huo haukufanyika hivyo mnapaswa kuandaa uchaguzi mwingine kujaza nafasi ya mwenyekiti ili ile dhana ya mara moja iliyoelezwa katika katiba yenu itekelezwe,” imesema barua hiyo.

Kupitia barua hiyo, Msajili amemtaka Kaimu Mwenyekiti Taifa TLP, kuitisha mkutano mapema iwezekanavyo ili uchaguzi wa kujaza nafasi hiyo ufanyike haraka iwezekamnavyo.


Hii ni mara ya pili kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, kuiandikia barua TLP ikiitaka uongozi wake ujieleze kwa nini umeshindwa kufanya uchaguzi huo.

Ni baada ya mkutano ulioandaliwa kufanya uchaguzi huo Machi 2023, kuahirishwa kwa madai ya kugubikwa na vitendo vya rushwa baina ya wagombea.

Makamu Mwenyekiti wa TLP, Hamad Mkadamu Rajabu, amesema utekelezaji wa agizo hilo amesema maandalizi yanafanyika hivyo uchaguzi huo unatarajiwa kufanywa Agosti mwaka huu.


“Hatujapanga siku gani utafanyika lakini tunatarajia mwezi Agosti utafanyika. Tutakaa hivi karibuni na Msajili wa Vyama vya Siasa kasha tutapanga namna ya kutekeleza agizo hilo,” amesema Mkadamu.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii