Azam FC, Singida BS kuanzisha timu za wanawake

Katika kuhakikisha Azam FC na Singida Big Stars zinakidhi kanuni za kushiriki Michuano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika msimu ujao 2023/24, Uongozi wa klabu hizo umeahidi kufanya mchakato wa kununua timu za wanawake, imeelezwa.

CAF ilitoa mwongozo unaozitaka timu zinazoshiriki mashindano yake kuanzia msimu wa 2023/24 lazima iwe na timu ya wanawake inayoshiriki mashindano yoyote katika nchi inayotokana na waraka huo umesisitizwa kuelekea maandalizi ya msimu ujao wa michuano ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika na Kombe la Shirikisho barani humo.

Taarifa kutoka CAF imesema hadi kufikia Juni 30, mwaka huu, itakuwa mwisho wa kutoa leseni kwa timu zinazoshiriki mashindano yake na kwa hapa nchini, tayari Young Africans na Simba SC wanauhakika wa kupata leseni hiyo kwa sababu wana timu za wanawake.

Mwenyekiti wa Singida Big Stars, Ibrahim Mirambo, amesema taarifa ya CAF wameiona na wanafanyia kazi ili kuhakikisha wanamiliki timu ya wanawake na hatimaye kupata leseni ya kushiriki michuano ya kimataifa msimu ujao.

Mirambo amesema mchakato wa kununua timu umeshaanza na wanahitaji kupata klabu ambayo itakuwa inashiriki Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania au Ligi ya Mabingwa wa Mikoa.

“Tumeanza kufuatilia, tutahakikisha kabla kufika hiyo tarehe husika, tutakuwa tumeshapata timu, hatuna mashaka kwa sababu tayari tuna timu ya mkoa ambayo tunamiliki na kama itakuwa ni lazima tuwe na klabu ya Ligi Kuu ya Wanawake, basi tutalazimika kununua timu nyingine kutoka katika daraja hilo,” amesema Mirambo.


Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii