Joao Cancelo awekwa sokoni kwa bei punguzo

Mabingwa wa Soka nchini England Manchester City wamekubali kushusha ada ya usajili ya kiungo wao Joao Cancelo na sasa ikiwa kuna timu inataka kumsajili katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi itatakiwa kulipa Pauni 35 milioni.

Cancelo ambaye msimu uliomalizika alikuwa akiichezea kwa mabingwa wa Soka nchini Ujerumani FC Bayern Munich kwa mkopo, huduma yake inahitaji sana na Arsenal na Barcelona.

Kiasi hicho cha Pauni 35 milioni, kimepunguzwa kutoka Pauni 60 milioni ambayo mabosi wa Man City walikuwa wakihitaji hapo awali na ikatajwa kama sababu ya Bayern kumkaushia.

Ikiwa haitapatikana timu iliyo tayari kutoa Pauni 35 milioni, Man City huenda ikamtumia Cancelo kama sehemu ya ofa ya kumpata Joshua Kimmich mwenye umri wa miaka 28.

Mkataba wa fundi huyu wa kimataifa wa Ureno unatarajiwa kumalizika mwaka 2027.

Msimu huu amecheza mechi 47 za michuano yote na kufunga mabao matatu.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii