MWEKEZAJI WILAYANI MKALAMA ADAIWA KUKITAPELI KIJIJI, ARDHI ALIYOPEWA KUWEKEZA SHULE AIKODISHA KWA KILIMO

MWEKEZAJI aliyetaka kujenga shule ya sekondari katika moja ya kijiji  wilayani Mkalama mkoani Singida anadaiwa kufanya utapeli baada ya ardhi aliyopewa na kijiji kwa ajili ya kujenga shule  kuigeuza matumizi na kuanza kukodisha watu kuendesha shughuli za kilimo kwa zaidi ya miaka 14.
Suala hilo limeibuliwa na wananchi wa Wilaya ya Mkalama kwenye kikao na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba ambaye anaendelea na ziara yake ya kutembelea kila wilaya kwa ajili ya kusikiliza kero na kuzipatia ufumbuzi.
Katika ziara hiyo wilayani humo Serukamba alipokea kero 49 huku kero 43 zikihusu migogoro ya ardhi kama mashamba, viwanja na nyumba.
Akizungumza baada ya kusikiliza kero hiyo Serukamba aliagiza ardhi hiyo irudishwe kwa halmashauri ya kijiji hicho kama sheria inavyoelekeza kuwa kama ardhi haijaendelezwa kwa muda mrefu inapaswa kurejeshwa kwa walengwa.
Kero nyingine iliyoleta msisimko kwenye kikao hicho ni ya serikali ya Kijiji cha Iglansoni kudaiwa kuipora familia ya mama Melisiana mashamba zaidi ya ekari 60 na kisha kuanza kuyakodisha kwa wananchi kwa ajili ya kuendesha shughuli za kilimo huku fedha zinazopatikana zikinufaisha viongozi wa kijiji hicho.
Serukamba alimuagiza Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Mkalama, Mkurugenzi na Afisa Ardhi wa Wilaya hiyo kwenda katika kijiji hicho na kufanya utaratibu wa kumrudishia mashamba mama huyo.
Katika hatua nyingine Maafisa ardhi, Watendaji waVijiji na Kata wilayani humo wametakiwa kuacha vitendo vinavyo sababisha migogoro ya ardhi ambayo imetajwa kama chanzo cha umaskini kwa wananchi na kuacha kushiriki vitendo vya uuzaji wa ardhi ambazo tayari zinaumiliki wa watu wengine na badala yake wajikite kuwashauri wananchi kuhusiana na mambo ya ardhi.
“Maafisa ardhi, watendaji wa kata na vijiji msiwe chanzo cha umaskini wa wananchi, watu wanataka kulima, kufanya maendeleo lakini mnawakwamisha mnaposhindwa kuwatatulia shida zao” alisema Serukamba.
Aidha Serukamba amewataka watumishi wilayani humo kutekeleza wajibu wao kikamilifu na kuwa kwa kufanya hivyo kutapunguza kero za wananchi.

Utaratibu huu ulioanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa kusikiliza kero za wananchi kila wilaya umepewa kongole na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mkalama James Mgwega ambaye alisema utasaidia kupata majawabu ya kero za muda mrefu za wananchi ambazo zilikaliwa na viongozi wa maeneo husika.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii