uwezo wa kuzaa kwa wanawake kushuka

 miaka 30 ijayo mwanamke wa Tanzania atakuwa na uwezo wa kujifungua wastani wa watoto wachache


 ripoti ya ‘Tanzania in figures 2021’ kuonyesha uwezo wa kuzaa wa wanawake nchini umeshuka kwa asilimia 18 ndani ya miaka 17.

Ripoti hiyo inayotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) imeonyesha kupungua uwezo wa kuzaa kwa wanawake kutoka wastani wa watoto sita 2004/2005 hadi 4.9 mwaka 2021.


Takwimu hizi zinamaanisha kila mwaka wanawake wa Tanzania wanapunguza idadi ya kuzaa watoto kwa asilimia moja.

Licha ya idadi hiyo kuzidi kushuka, kwa upande wa Tanzania bara takwimu zinaonyesha wanawake wa vijijini bado wana uwezo mkubwa wa kupata watoto wengi hadi kufikia sita ikilinganishwa na wale wa mijini ambao hupata watoto wanne tu, ikiwa ni tofauti ya watoto wawili.

Daktari wa magonjwa ya ndani Hospitali ya Taifa ya Muhimbili-Mloganzila, Innocent Tesha alisema sababu kubwa ya uzazi wa wanawake wa mijini kuwa wa kiwango cha chini ni pamoja na mfumo wa maisha wanayoishi.

“Mfumo wa maisha unaanzia kwenye ulaji wa chakula, muda wao katika familia na matumizi ya kemikali kwenye ulaji na urembo. Kwa upande wa vijijini wanawake wana mazoezi ya kila aina, yakiwamo ya kutembea, kufanya kazi na hata lishe yao ni tofauti na wa mjini,” alisema Dk Tesha.

“Lakini mijini kama mtu hana gari anapanda mwendokasi, kwa hiyo mfumo wa maisha bwete unafanya mishipa ya damu kushindwa kuwa na msaada kwenye masuala ya uzazi.”


Dk Tesha akizungumzia ulaji alisema, wanawake wa vijijini wanakula vyakula asili vyenye virutubishi muhimu kwenye utengenezaji wa mimba, huku wanawake wa mjini wakiwa waathirika wa vyakula vilivyokwisha kuandaliwa haraka ambavyo havina msaada wowote kwenye utungishwaji wa mimba ya mtoto.

Kwa upande wake, Dk Edson Francis alisema wanawake wa mjini wanaogopa maumivu ya kuzaa kwa njia ya kawaida na wengi wanakimbilia kufanyiwa upasuaji ambao unakuwa na ukomo wa idadi ya watoto.


“Kwa mazingira ya mjini wanawake wengi wanatumia mfumo wa maisha ya magharibi, utakuta muda wa kuzaa atazaa lakini ataomba kuzaa kwa upasuaji, sasa mwanamke yeyote anayejifungua kwa upasuaji uzazi wake unakuwa na ukomo,” alisema Dk Francis.

“Ukifanyiwa upasuaji watoto tunashauri mwisho watatu, sasa wanawake wa mijini wanaepuka maumivu wakati wa uzazi kwa njia ya kuomba kufanyiwa upasuaji, tofauti na wa vijijini.”

Jambo lingine alilotaja Dk Francis ni matumizi ya dawa za kuzuia mimba ambazo zimekuwa zikitumiwa zaidi na wanawake wa mijini na huathiri homoni na kuchangia mwanamke kuwa na mtoto mmoja au wachache kulinganisha na vijijini.

Daktari kutoka Kituo cha Afya Haffarod Health Clinic ya Temeke, Ford Chisongela alisema uwezo mkubwa wa wanawake wa vijijini kuwa na watoto wengi ikilinganishwa na wa mijini inatokana kuwa mbali na njia za uzazi wa mpango.

“Pia, wanapata muda mwingi kuwa na wenza wao, jambo lingine utamaduni, wanaona ni fahari kuwa na watoto wengi,” alisema.

Dk Chisongela alisema umaskini unaweza kuchangia wanawake wa vijijini kushindwa kufikia huduma nyingi za afya, hali ambayo huwa na matokeo makubwa kwenye ongezeko la uzazi.

Alitaja ukosefu wa elimu, utamaduni maeneo ya vijijini kuwa na matokeo makubwa kwenye ongezeko la kuzaliana vijijini.

“Kwa watu wa mijini muda mwingine wanachelewa kupata watoto kutokana na kutumia muda mwingi kwenye kusoma, pia wanaume wenyewe hawapendelei kuoa wanawake ambao wamewazidi kipato, hilo linaweza kuchangia pia,” alieleza.

Dawa kunogesha tendo la ndoa

Mkazi wa Mabibo, Dar es Salaam, Veronica Magonjeka alisema wanawake wengi wa mjini wanasumbuliwa na uzazi kwa sababu ya dawa za kuongeza utamu wa tendo la ndoa ambazo nyingi wanazinunua mitandaoni.

“Sasa hivi ukiingia kwenye mitandao ya kijamii unakuta kuna watu wanajiita makungwi ambao wanauza dawa za kuongeza utamu wa tendo la ndoa, mara nyingi maelezo yake ni kuziweka sehemu za siri, kitu ambacho nahisi kina madhara,” alisema Veronica.

Mkazi wa Temeke, Aisha Zuberi alisema, kulingana na hali ya maisha ni nadra mtu kuwa na watoto wengi huku akiwa na kipato chenye shaka.

“Umaskini ni mkubwa kwenye familia nyingi, ukisema uwe na watoto watano utawapa nini, wanaume wengine kwanza kutoa matunzo ya mtoto mmoja wanakimbia,” alisema Aisha.


Kutokana na hali hiyo, Aisha alisema wanawake wengi wamekuwa watafutaji zaidi ya wanaume, hivyo muda mwingi utatumika kutafuta badala ya kujenga familia.

“Ukienda Soko la Tandika, Manzese au kokote asubuhi sana utawakuta wanawake na mizigo ya biashara, ukienda vijijini mwanamume kwa kiwango kikubwa ndiye anayewajibika, kama mwanamke atashiriki, ni kwenye shughuli za nyumbani, hivyo lazima apate muda wa kutosha kuwa na mwenzi wake,” aliongeza.


Hali ilivyo vijijini

Naisioki Mollel, mkazi wa Sekei wilayani Arumeru mkoani Arusha alisema wanawake wengi wa vijijini wanakubali kuzaa watoto kwa sababu wana muda wa kutosha kuwalea.

“Huko mjini wengi wanatumia wasaidizi wa kazi za ndani kwenye malezi wao, wanakwenda kuhangaika kutafuta hela, sisi kwetu huku ni tofauti, tunaangalia zaidi kuongeza familia na hatuhofii suala la mali kwa sababu tuna mashamba, tofauti na wenzetu (wakazi wa mjini),” alisema Mollel.


Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii