Shirika la Kimataifa la kutetea haki za binadamu lililo na makao yake mjini London Amnesty International, limesema kuwa vikosi vya Ukraine vinakiuka sheria za kimataifa na kuhatarisha raia kwa kuweka kambi katika maeneo ya makazi, ikiwa ni pamoja na shule na hospitali. Madai hayo yamesababisha majibu ya hasira kutoka Ukraine. Ukraine imesema kuwa shirika hilo la haki linaelezea kile ilichokiita usawa wa uwongo kati ya hatua za majeshi ya uvamizi ya Urusi na Waukraine kutetea nchi yao. Katika hotuba yake ya kila siku hapo jana, rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema kuwa Amnesty imejaribu kulihurumia taifa la kigaidi na kuelekeza lawama kutoka kwa mchokozi hadi kwa mwathiriwa na kuongeza kuwa hakuna hali ya uvamizi wowote wa Urusi kuelekea Ukraine inayoweza kuhalalishwa. Zelensky ameongeza kuwa uchokozi dhidi ya taifa lake haukuchochewa, ni uvamizi na ugaidi.