Mahakama ya Sweden yamuhukumu kifungo cha maisha jela afisa wa zamani wa Iran

Mahakama moja ya wilaya mjini Stockholm, Sweden, Alhamisi imemuhukumu afisa wa zamani wa Iran kifungo cha maisha jela kwa uhalifu wa kivita na mauaji ya wafungwa wa kisiasa wakati wa vita kati ya Iran na Iraq mwaka wa 1980.

Wakati wa mauaji hayo, Hamid Noury alikuwa na umri wa miaka 27 na mshauri wa naibu mwendesha mashtaka kwenye gereza la Gohardasht huko Karaj, nchini Iran.

Kwa mujibu wa waendesha mashtaka, mauaji hayo yaliamrishwa na Ayatollah Khomeini, kiongozi wa Iran wakati huo. Wafungwa walionyongwa walikuwa watiifu kwa kundi la upinzani la Iran, Mujahedeen-e-Khalq, linalojulikana kama MEK.

Noury, ambaye sasa ana umri wa miaka 61, alikamatwa alipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Stockholm mwaka wa 2019. Alikanusha shutma dhidi yake.

Mahakama hiyo ya Sweden imesema inaamini kunyongwa kwa wafungwa hao ulikuwa ukiukaji mkubwa wa sheria ya kimataifa ya kibinadamu kutokana na mzozo wa kivita wa kimataifa.

Wizara ya mambo ya nje ya Iran inaamini kuwa hukumu hiyo “imechochewa kisiasa na haina uhalali wa kisheria”, msemaji wa wizara hiyo Nasser Kanaani amesema katika taarifa.

Noury anaweza kukata rufaa dhidi ya hukumu hiyo. Akiachiwa huru, atafukuzwa Sweden.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii