Rais wa China amwapisha kiongozi mpya Hong Kong

Rais wa China, Xi Jinping leo amemwapisha kiongozi mpya wa Hong Kong huku akionya kuwa China haitavumilia upinzani wowote dhidi ya mamlaka yake katika eneo hili.

Kiongozi huyo ni wa kwanza mwanamke wa Hong Kong anayefahamika kwa jina la Carrie Lam.

Katika hotuba yake yenye maneno makali wakati wa kuadhimisha miaka 20 tangu koloni hilo la zamani la Uingereza kurejea kwa China, Jinping amesema juhudi zozote zinazofanywa na baadhi ya watu nchini kupinga mamlaka ya China hazitakubalika.

"Juhudi zozote zinazoweza kuhatarisha uhuru na mipaka  ya China pamoja na usalama wake, ni sawa na  kupambana na dola ya serikali kuu ya China na mamlaka  ya sheria mama au kuitumia Hong Kong kuingiza mambo au shughuli za kuhujumu bara kitakuwa kitendo cha kuvuka mstari mwekundu,” amesisitiza.

Chini  ya  katiba  ndogo  ya  Hong Kong , sheria  ya  msingi, jimbo hilo ambalo ni sehemu muhimu ya  kiuchumi inahakikishiwa uhuru wake kwa takriban miaka  50 baada ya mwaka 1997.

Hong Kong ni jimbo maalumu la utawala ambalo  linaongozwa chini ya utaratibu wa "nchi moja, mifumo miwili" unaoruhusu mamlaka makubwa ya ndani.


Jinping alikuwa akihutubia ukumbi uliojaa wageni  waalikwa pamoja na watu mashuhuri wengi wao wakiwa  ni waungaji mkono Serikali kuu mjini Beijing.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii