Sudan iko kwenye mazungumzo ya kutatua mzozo wa kisiasa

Sudan Jumatano imeanzisha mazungumzo ya moja kwa moja na makundi hasimu chini ya upatinishi wa Umoja wa mataifa ikitumai kutatua mzozo wa kisiasa uliochochewa na mapinduzi ya kijeshi ya mwaka jana, lakini muungano mkubwa wa mashirika ya kiraia umesusia mazungumzo hayo.

Tangu kufanyike mapinduzi ya kijeshi, Sudan imekumbwa na mzozo mkubwa, maandamano ya kila wiki, ukandamizaji mbaya ambao uliua zaidi ya watu 100, na uchumi wake kuzidi kudorora.

Huku mazungumzo hayo yakifanyika katika mji mkuu Khartoum, mamia ya watu walikusanyika mashariki mwa mji huo wakiomba utawala wa kiraia, katika maandamano ya hivi karibuni dhidi ya mapinduzi ya tarehe 25 Oktoba yaliyoongozwa na mkuu wa jeshi Abdel Fattah al-Burhan.

Maafisa wa usalama walifyatua gesi ya kutoa machozi kutawanya waandamanaji hao, mwandishi wa habari wa AFP aliyefika kwenye eneo la tukio amesema.

“Ni muhimu kutoruhusu fursa hii ipotee,” mwakilishi maalum wa Umoja wa mataifa Volker Perthes amewambia waandishi wa habari mjini Khartoum.

“Tunaomba kila mtu afanye kazi na mwingine kwa nia njema.”

Mapinduzi ya kijeshi yalidhoofisha utawala wa mpito wa kiraia ambao ulianzishwa kufuatia kuondolewa madarakani kwa kiongozi wa muda mrefu Omar al-Bashir mwaka wa 2019.

Umoja wa Afrika na jumuia ya IGAD tangu mwezi Machi wamekuwa wakiushinikiza uongozi wa Sudan kufanya mazungumzo ili kumaliza mzozo wa kisiasa.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii