Niger yaruhusu chanjo ya malaria kwa watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano

Niger imeruhusu chanjo dhidi ya malaria iliyotengenezewa Uingereza itolewe kwa watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano, ili kupambana na ugonjwa huo ambao uliua zaidi ya watu 4,000 nchini humo mwaka wa 2021, waziri wa afya ameiambia AFP Alhamisi.

“Serikali ya Niger imetoa ruhusa kwa matumizi ya chanjo dhidi ya malaria kwa watoto wa miaka sufuri hadi mitano” ambao ndio huathiriwa zaidi na ugonjwa huo kila mwaka, waziri wa afya Illiassou Mainasara, ameiambia AFP.

“Katika miezi ijayo, chanjo hiyo itawasili nchini na hatua zote zimechukuliwa ili kufanikisha mpango huo,” amethibitisha waziri huyo wa afya.

Tarehe 9 Oktoba mwaka wa 2021, shirika la afya duniani ( WHO) lilipendekeza chanjo hiyo aina ya RTS -S ya kampuni kubwa ya Uingereza GSK, itolewe kwa wingi kwa watoto ili kupunguza kwa kiasi kikubwa ugonjwa wa malaria.

Tangu mwaka wa 2019, Ghana, Kenya na Malawi zilianza kutoa chanjo hiyo katika baadhi ya maeneo.

Zaidi ya watoto milioni 1 wamekwisha pata chanjo hiyo katika nchi hizo, ikionyesha kupunguza kwa kiasi kikubwa visa vikali vya malaria, kulingana na WHO.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii