Ukraine yasema maelfu ya watu wameuawa Mariupol

Mamlaka nchini Ukraine zimesema huenda maelfu ya watu wameuawa kufuatia mashambulizi ya Urusi katika mji wa bandari wa Mariupol, na kuishtumu Urusi kuchelewesha kimakusudi zoezi la kuhamisha watu kutoka mji huo uliozingirwa, ambao unatajwa kuwa uko hali mbaya. Katika ujumbe wake kwa njia ya video kwa bunge la Korea Kusini, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenksiy amesema mji wa Mariupol umeharibiwa, na kwamba maelfu ya watu wamekufa lakini licha ya hayo, Urusi bado inaendeleza mashambulizi yake. "Katika maeneo yaliyochukuliwa na Urusi, jeshi la nchi hiyo kwa makusudi limewalenga waalimu, watu wanaohusika na jeshi la Ukraine na utendaji wa serikali, wanaharakati, waandishi habari. Watu ambao wanaelimisha jamii na kutetea umoja wa kitaifa. Watu wa aina hiyo walitekwa nyara, waliuawa kwa makusudi. Hiyo ilikuwa ni amri, ilikuwa ni mbinu."Shirika la habari la Reuters limethibisha uharibifu mkubwa katika mji huo lakini halikuweza kuthibitisha idadi kamili ya watu waliokufa katika mji huo wa kimkakati, ulioko kati ya Crimea inayodhibitiwa na Urusi na maeneo ya mashariki mwa Ukraine yanayoshikiliwa na wapiganaji wanaotaka kujitenga na ambao wanaungwa mkono na Urusi.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii