Mpigania uhuru Muthoni Wa Kirima, mwenye umri wa miaka 92, amefafanua sababu za kumruhusu aliyekuwa mama wa taifa, Mama Ngina Kenyatta, kunyoa nywele zake za rasta.
Baada ya kuzifuga nywele zake za rasta kwa zaidi ya miaka 70, kama ushuhuda wa kupigania uhuru, Muthoni alizikata Jumamosi, Aprili 2.
Mama Ngina aliongoza sherehe hiyo, huku wawili hao wakikumbuka maisha yao ya ujana, urafiki na kupigania uhuru.
Shujaa huyo alijitokeza Jumatatu, Aprili 4, siku mbili baada ya hafla hiyo kuzima uvumi kwamba Mama Ngina alimlazimisha kunyoa rasta zake zenye urefu wa futi sita.
Muthoni alisisitiza kwamba aliamua kunyoa nywele zake ili kuashiria kwamba Kenya imepata uhuru kamili.
Alieleza kuwa alimchagua Mama Ngina kukata nywele zake kwa hiari yake mwenyewe.
"Ilinibidi nizikate kwa sababu imekuwa safari ndefu. Nilianza kutunza nywele hizi mwaka wa 1952 na baada ya zaidi ya miaka 70, nilihitaji kupumzika na kufurahia kunyoa. Ninahisi kama msichana mdogo sasa," Kirima alisema.
Aliongeza kuwa: "Hakuna mtu anayeweza kuninyoa bila idhini yangu. Kama wangejaribu kufanya hivyo, ningewapiga mangumi na mateke."
Uamuzi wa kuweka rasta uliashiria uvumilivu mwingi aliopitia chini ya utawala mbaya wa kikoloni.
"Dreadlocks ndio mtindo wa nywele unaohusishwa na Mau Mau walipokuwa wakipigana msituni kwani hawakuwa na wakati wa kutunza nywele zao vizuri, na kuzifunga," Muthoni alisema.
Muthoni alichangia vipi Kenya kupata uhuru?
Muthoni alichangia pakubwa katika kupigania uhuru wa Kenya.
Mpiganaji huyo aliishi miaka saba msituni kama mmoja wa wapiganaji wa Mau Mau akiwa kwenye mstari wa mbele katika vita vya kupigania uhuru.
Tofauti na wanawake wengine ambao walipewa majukumu ya kijasusi na kupeleka chakula, Muthoni alihusika kikamilifu katika vita vya kweli msituni.
Zoezi la unyoaji lilifanywa baada ya mkutano wa faragha kati ya Mama Ngina na wazee wengine wa kimila nyumbani kwake eneo la Tatu, mjini Nyeri.
Katika hotuba yake, mamake rais alihimiza eneo la Mlima Kenya kuungana na kuacha kurushiana matusi.
Katika mkutano huo uliofanyika Nyeri, wapigania uhuru wengine walitoa malalamishi yao na changamoto zinazowakabili licha ya kuwa raia waanzilishi wa nchi.