Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Hungary imeanzisha uchunguzi wa tuhuma za ubadhirifu wa fedha na makosa ya jinai, wakivamia kituo cha data cha chama cha Viktor Orbán.
Mawakili wa serikali nchini Hungary wamevamia kituo kinachohifadhi data za chama cha Fidesz cha aliyekuwa Waziri Mkuu Viktor Orbán, ikiwa ni sehemu ya uchunguzi wa tuhuma za ubadhirifu wa fedha na makosa mengine ya jinai.
Ofisi ya Mwendesha Mashtaka ya Kaunti ya Bács-Kiskun imethibitisha kuendelea kwa uchunguzi huo, lakini imesema haiwezi kutoa maelezo zaidi kwa sasa ili kutoathiri mwenendo wa kesi hiyo.
Kwa upande wa chama cha Fidesz, wachunguzi walifika bila taarifa katika kituo kinachohifadhi mifumo yake ya mawasiliano na hifadhidata, wakinuia kukamata mfumo mzima wa mawasiliano wa chama hicho.
Kupitia taarifa iliyochapishwa kwenye Facebook, Fidesz imedai kuwa hatua hiyo haijawahi kushuhudiwa nchini Hungary tangu kumalizika kwa utawala wa kikomunisti mwaka 1990.
Serikali ya Waziri Mkuu Peter Magyar imekuwa ikitekeleza mageuzi makubwa ya kupambana na rushwa na kuondoa ushawishi wa viongozi wanaodaiwa kuwa waaminifu kwa utawala wa Orbán.