Jela Miaka 30 Kwa Kumbaka Kiziwi Wilaya ya Kwimba, Mwanza

Mahakama ya Wilaya ya Kwimba, mkoani Mwanza, imemhukumu Malimo Mathias Nguno maarufu kama Gohe (41), kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka mtoto mwenye umri wa miaka 13 ambaye pia ni mlemavu wa kusikia (kiziwi).

Hukumu hiyo imesomwa Aprili 08, 2025, na Hakimu Mfawidhi Ndeko Dastan Ndeko, ambaye amesema kuwa mahakama imeridhishwa na ushahidi uliowasilishwa na upande wa Jamhuri katika kesi ya jinai namba 2904/2025. Mshtakiwa amepatikana na hatia chini ya vifungu vya sheria namba 130(1)(2)(e) na 131(1) vya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16, marejeo ya mwaka 2022.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, tukio hilo lilitokea Januari 4, 2025, katika Kijiji cha Nyambuyi, Wilaya ya Kwimba, kwa mtoto mwenye ulemavu wa kusikia na kuongea.

Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Juma Kipalo, alisema kuwa mshtakiwa alifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza Februari 4, 2025, ambapo alikana mashtaka. Upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi watano wakiwemo mwalimu na mtaalam wa lugha ya alama aliyemsaidia mhanga kueleza kilichotokea.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii