Shambulizi la Israel laua wanahabari watano huko Gaza

Madaktari wa Palestina wamesema shambulizi la Israel mapema Alhamisi limewaua wanahabari watano katika kambi ya Nuseirat katikati mwa Gaza.

Kituo cha Televisheni cha Al-Quds, chenye uhusiano na kundi la wanamgambo la Islamic Jihad, kimesema katika taarifa kwamba shambulizi hilo lilipiga gari la kituo hicho na kuwaua wafanyakazi wake watano.

Al-Quds imesema wanahabari hao waliuawa “wakati wakifanya kazi yao ya uandishi na ubinadamu.”

Jeshi la Israel limesema wanajeshi wake walilishambulia gari ambalo walikuwemo magaidi wa Islamic Jihad katika eneo la Nuseirat.

Wakati huo huo, mtoto mchanga wa kike alifariki kutokana na baridi kali kusini mwa Gaza, mkuu wa wizara ya afya katika eneo hilo alisema Jumatano. Mtoto huyo mchanga ni wa tatu kufariki katika siku za hivi karibuni kwasababu ya baridi.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii