Tume Ya Uchaguzi Ya DRC Yafuta Kura Za Baadhi Ya Wagombea Wa Ubunge Na Udiwani

Tume ya uchaguzi ya Congo imesema kwamba imefuta kura zilizopigiwa wagombea 82 kati ya 101,000 waliowania viti vya bunge na udiwani, kwenye uchaguzi mkuu uliyofanyika Desemba.

Hatua hiyo ni kutokana na madai kwamba walihusika katika udanganyifu pamoja na masuala mengine ya kuvuraga zoezi hilo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, miongoni mwa walioathiriwa ni pamoja na wagombea wa mabaraza ya majimbo na manispaa, na ambao matokeo yao bado hayajatangazwa.

Hata hivyo taarifa hiyo ya Ijumaa kutoka tume ya uchaguzi ya CENI, haikutaja lolote kuhusiana na uchaguzi wa rais uliozua utata pia, baada ya Rais Felix Tshisekedi kutangazwa mshindi Jumapili iliyopita. Upinzani umepinga matokeo hayo ukidai kwamba kulikuwa na dosari nyingi wakati wa zoezi hilo.

Hatua hiyo inahofiwa kuyumbisha zaidi taifa hilo lenye utajiri mkubwa wa madini, na ambalo tayari limetatizika.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii