Mahakama ya Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma imewahukumu kifungo cha Miaka 30 Mussa Zuberi Amuri (28) na Saidi Shaibu Saidi (27) wote wakazi wa Kijiji cha Lukumbule Wilaya ya Tunduru baada ya kupatikana na hatia kwa kosa la unyang’anyi wa kutumia nguvu.
Akisoma hukumu hiyo ya kesi ya Jinai Na 59 ya mwaka 2023, Hakimu mkazi wa Mahakama, Kando alisema Mahakama imefikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha na ushahidi uliotolewa pasi na shaka, ambapo Watuhumiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo Februari 27, 2023 na kufikishwa mahakamani Machi 9, 2023 ambapo Novemba 2, 2023 hukumu ilitoka na wakapatikana na hatia ya kosa hilo.
Aidha, katika hukumu nyingine mkazi wa Kijiji cha Nyamizeze Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza, Samson Mibulo (35), naye amehukumiwa kwenda jela miaka 30 baada kukiri kosa la kubaka baada ya kukumbwa na kesi hiyo ya jinai namba 122/2023, hukumu iliyotolewa Novemba 2, 2023 na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Sengerema, Evod Kisoka.