Zaidi ya Watu 50 Wafariki Katika Mlipuko wa Lori la Mafuta

Zaidi ya watu 50 wamefariki dunia na wengine kujeruhiwa kwa kuungua na moto vibaya, baada ya lori la mafuta kulipuka katika kijiji kimoja  kilichopo Magharibi mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Paris today, baadhi ya majeruhi wa ajali hiyo hali zao ni mbaya sana na kuna uwezekano wa idadii ya vifo kuongezeka.

 

Aidha, taarifa hiyo inaeleza mlipuko huo ulitokea usiku wa kuamkia Septemba 15, 2022 katika kijiji cha Mbuba kilichopo kilomita 120 Magharibi mwa Mji wa Kinshasa nchini humo.

 

Tukio jingine kama hilo lilitokea mwaka 2018 ambapo zaidi ya watu 50 walifariki katika kijiji hicho kilichopo kwenye barabara kuu ya RN1 yenye shughuli nyingi inayounganisha Mji wa Kinshasa na Bandari ya Matadi na Boma.

Mwaka 2010 takribani watu 230 walipoteza maisha nchini humo, baada ya lori la mafuta kupinduka na kulipuka kisha moto kusambaa katika makazi ya watu na kumbi za sinema zilizokuwa zimefurika watu waliokuwa wanaangalia fainali za Kombe la Dunia.

 

Matukio kama haya yamekuwa yakitokea mara kwa mara katika mataifa ya Magharibi mwa Afrika na kusababisha makumi ya watu kupoteza maisha yao na wengine kupata vilema vya maisha.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii