Viongozi wa kijeshi nchini Chad wamepiga marufuku maandamano ya upinzani yaliyopangwa baadaye wiki hii, kwa madai ya kuchelewa kuwasilisha maombi kwa wakati, kulingana na taarifa iliyotolewa Jumatano.
Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, muungano wa vyama vya upinzani pamoja na asasi za kiraia, wa Wakit Tamma ulikuwa umeitisha maandamano Ijumaa dhidi ya baraza la kijeshi la mpito linalotawala, na linaloongozwa na generali Mahamat Idriss Deby.
Lengo la muungano huo lilikuwa kuanza maandamano siku moja kabla ya kuanza kwa kile kilichotajwa kuwa mjadala wa kitaifa siku ya Jumamosi, kwa lengo la kupanga mikakati kuelekea kwenye uchaguzi mkuu na kurejesha utawala wa kiraia. Kundi la Wakat Tamma limekataa kushiriki kwenye mazungumzo hayo ambayo yanawaleta pamoja maafisa wa serikali, vyama vya wafanyakazi, upinzani pamoja na asasi za kiraia.
Muungano huo kupitia taarifa ya pamoja umesema kwamba baraza la kijeshi limepanga kuitisha mazungumzo yanayoegemea upande mmoja kwa kuvitenga vyama vya upinzani vyenye nguvu pamoja na mashirika mengine ya kiraia.