WATU WAWILI WANASWA WAKISAFIRISHA POMBE HARAMU KWA KUTUMIA GARI LA KUBEBEA MAITI.

Watu wawili wametiwa mbaroni kwa madai ya kusafirisha pombe haramu iliyovishwa kama maiti kutoka eneo la Magharibi mwa Kenya hadi Nairobi wakitumia gari la kubebea maiti.
Wawili Wanaswa Wakisafirisha Chang’aa kwenye Gari la Kubebea Maiti
Baada ya kusafiri kwa zaidi ya kilomita 200, maafisa wa polisi kutoka Kabete walikamata gari la kubeba maiti katika eneo la Uthiru, Jumanne, Mei 17.
Akithibitisha kisa hicho, OCPD wa Dagoretti Francis Kinyua alisema baada ya msako chini ya gari hilo ambapo kawaida maiti huwekwa wakati wa usafirishaji, walipata lita 130 za pombe haramu.
"Baada ya upekuzi wa kina chini ya utumbo wa gari, tulipata lita 130 za pombe haramu ya Chang’aa waliyokuwa wakisafirisha kinyume cha sheria. Kufikia sasa tumewakamata watu wawili,” Kinyua alisema.
Kinyua alisema pombe hiyo haramu ilikuwa imewekwa kwenye mifuko ya plastiki ambayo iliwekwa katikati ya mahindi yaliyokaushwa ili kuzuia harufu yoyote.
Mkuu huyo wa polisi alitoa wito kwa maafisa wa usalama kuwa makini na kufanya upekuzi kila mara kwenye gari la kubebea maiti na gari la wagonjwa kwa sababu wengi wanafanya biashara ya kusafirisha vitu haramu na dawa za kulevya wakitumia magari hayo.
"Ninawaomba maafisa wa kutekeleza sheria kufanya msako wa papo kwa papo katika magari haya ili kupata washukiwa zaidi na kukomesha uovu huo," Kinyua aliongeza.
Washukiwa hao wawili wako katika seli ya polisi wakisubiri kufikishwa mahakamani huku polisi wakiendelea na uchunguzi zaidi.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii