PANYA ROAD WAPEMA ONYO.

Mawaziri Dkt. Dorothy Gwajima wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Hamadi Masauni wa Mambo ya Ndani ya Nchi, wameuambia umma kuwa, vijana wadogo wanaovamia watu na kuwakata kwa silaha zenye ncha kali kisha kuwa pora hawana uwezo wa kushindana na serikali iwapo wananchi watakuwa bega kwa bega katika kutoa taarifa za Uhalifu na viashiria kwa mamlaka za Serikali.

Wakizungumza hapo jana, Mei 18, 2022, Jijini Dar es Salaam kwenye kata za Chanika, Zingiziwa na Buza jijini humo wamesema, uwepo wa Mshikamano wa wanajamii na Serikali ndio suluhu ya kutokomeza vikundi hivyo vya vijana wanakadiriwa kuwa na miaka kati 16 hadi 20 kiasi.

Akizungumza kwenye Mkutano wa Hadhara, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, alisema kumomonyoka kwa maadili katika makuzi na malezi ndio chanzo kikuu cha uzalishaji wa Kundi hilo.

“Mpaka mtoto anakuwa hivyo, sio suala la usiku mmoja, unakuta anaanza kidogo kidogo na ninyi wazazi kwakuwa hamtengi muda wakuzungumza naye na kujua mienendo yake, anazidi kukuwa na tabia hiyo hadi anafikia hatua sasa yakujiunga kwenye makundi ya kihalifu kama hilo la Panya Road” alisema Dkt. Gwajima

Waziri Gwajima, ameonya baadhi ya wanajamii kuacha kumuangalia mtoto kwa niwa mtu mwingine na badala yake watoto wote wahesabike kuwa wanajamii, kwani katika malezi ya sasa, baadhi ya wazazi hupandwa na hasira mwanae anapo adhibiwa au kuonywa na mzazi mwingine hali inayo nyong’onyeza jitihada za malezi na makuzi.

“Yapata juma moja nilikuwa eneo la Mbezi Luis, wazazi waliweka bayana haya mambo, wakisema, malezi ya zamani yalishirikisha jamii nzima, lakini kwa nyakati za sasa, wazazi wengi huweza kukufokea pale unapojaribu kumuongoza mwanane kwenye maadili mema, hii sio sawa kwani kufanya hivyo, huyo huyo mwanao Pamoja na wewe kujenga Gorofa kutokana na kutokuwa na malezi bora Mwanao mwenyewe anaweza kukuchinja kwenye nyumba yako. Alisisitiza Dkt. Gwajima.

Naye Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Hamadi Masaun, akiongea kwenye Mkutano huo ambao pia ulishirikisha Viongozi wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, alisema amefarijika kusikia tayari vijana zaidi ya 61 wakiwa wanashikiliwa na jeshi la Polisi kutokana na Ushirikiano ulioneshwa na Jamii.

“Mwanzoni nilipokuja hapa kila mmoja wetu alikuwa na sura ya simanzi kutokana na hofu na woga ulikuwa umetanda, lakini leo mmeniambia tayari wapo ambao wanashikiliwa na vyombo vya dola, lakini wengine tayari wamefikishwa Mahakamani kwa ajili yakukabiliana na kesi zao, niwapongeze sana kwa hili” alisema Masauni.

Naye Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro, alisema, kama Jeshi la Polisi kwenye Kanda hiyo wataendelea kufanya kazi kwa mujibu wa viapo vyao na hawata muonea muhali mtu yeyote ambaye atathubutu kucheza na Amani ya Mtanzania yeyote kwenye kanda hiyo.

“Tumefanya kazi kwa ukaribu sana na Polisi Jamii, hawa wamekuwa msaada mkubwa na kutuwezesha kuwapata baadhi ya wahalifu hao katika maeneo ya Chanika, Kunduchi Mtongani na Nyatira, ambapo baadhi ya watu waliokamatwa walikutwa na TV, Simu na vitu vingine vilivyo porwa kwenye matukio hayo.” Alisema Kamanda Muliro.

Nao wananchi wa Maeneo ya Chanika na Kata ya Buza hawakusita kuonesha furaha yao baada yakuwaona Mawaziri hao huku wakiwasifu na kumshukuru Waziri Gwajima kwa darasa la kamati za MTAKUWWA na majukumu yake.

Mawaziri Dkt. Gwajima na Masauni, kwa Pamoja na Kamanda wa Polisi kanda Maalum ya Dar es Salaam, walifanya ziara kwenye Kata za Chanika, na Buza na kuongea na wahanga wa matukio ya Panya Road yaliyokithiri kwenye jiji hilo ndani ya majuma mawili yaliyopita.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii