Mama mmoja alizua kizaazaa katika mahakama ya Eldoret nchini kenya baada ya kumlilia hakimu kumfunga mwanawe hadi pale ambapo yeye na mumewe watakapoaga dunia.
Sally Rotich alikuwa akizungumza mahakamani wakati wa kukana au kupinga mashtaka kwa Nelson Kiptoo Limo, ambaye ni mvulana wao wa pekee na aliyeshtakiwa kwa makosa ya kutishia kumuua mamake kwa upanga.
Katika kikao hicho cha Jumatano, Mei 11, akibubujikwa na machozi, Rotich alimsimulia Hakimu Mkuu Mkaazi Christine Menya jinsi Limo wamekuwa akiwahangaisha pamoja na majirani.
Alifafanua kuwa mwanawe mwenye umri wa miaka 33 amekuwa akiwapiga mara kwa mara pamoja na mumewe mwenye umri wa miaka 60 ambaye alilazimika kukimbilia Mombasa vichapo vya mwanao vilipozidi.
Mama huyo aliendelea na kuiambia kuwa mwanao alikuwa bado hajabadilika licha ya kutumikia kifungo cha miaka miwili kwa kuwapiga.
Kutokana na hali hiyo, Rotich aliitaka mahakama kumfunga Limo hadi pale ambapo watafariki ili waishi kwa amani kwa miaka yao iliyobaki.
“Ninaomba mahakama hii kutomwachilia mvulana huyu. Maisha yangu yako hatarini kutokana na vitisho na mashambulio ya mshtakiwa. Ninaomba mtuhumiwa kusalia gerezani hadi vifo vyetu ili tufurahie amani.
Iwapo ataachiliwa kabla ya vifo vyetu, atatuua,” Rotich amenukuliwa na gazeti la Daily Nation.Hata hivyo mshtakiwa alikanusha mashtaka hayo na kupinga madai ya mamake huku kesi hiyo ikiratibiwa kutajwa tena Mei 23.