Akamatwa na Bomu katika Uchaguzi wa Chama cha NRM, Uganda

Polisi nchini Uganda wanamshikilia mwanaume mmoja baada ya kukutwa na bomu la mkononi aina ya “guruneti” (Grenade) wakati wa uchaguzi wa awali wa chama tawala cha NRM .

Kwa mujibu wa NTV Uganda, tukio hilo limetokea eneo la Kamubezi lililopo Isingiro Kusini nchini humo, ambako taratibu za uchaguzi wa ndani wa chama hicho tawala kinachoongozwa na rais Yoweri Museven ulikuwa ukiendelea mapema leo hii.

Inadaiwa kuwa, mwanaume huyo ambaye jina lake halijawekwa wazi mpaka hivi sasa, ni miongoni wa wafuasi wa kambi ya mtia nia wa nafasi ya ubunge katika chama hicho anayefahamika kwa jina la Maari Mujuni, na alikuwa na dhumuni la kuvuruga zoezi hilo ambalo linawahusisha watia nia wengine ambao ni Alex Bakunda, Gilbert Rwabambari na Rudoviko Byarugaba

Aidha katika uchaguzi huo ambao unalenga kuwapata wagombea mbali mbali watakaopeperusha bendera ya chama cha NRM (National Resistance Movement) katika Uchaguzi mkuu ujao, kumeripotiwa matukio mbali mbali yanayohusisha vurugu katika maeneo tofauti, huku vyombo vya usalama vikitoa onyo kali kwa watakaovuruga amani kupitia zoezi hilo

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii