Mahakama ya Misri yatoa hukumu ya kifo kwa wanamgambo 10 wa kiislamu

Mahakama moja ya Misri Jumanne imewahukumu kifo wanamgambo 10 wa kiislamu waliokutwa na hatia inayohusiana na vitendo vya ugaidi chanzo cha mahakama kimesema.

Wanaume hao ambao walishtakiwa kwa kuongoza kundi lijulikanalo kama Helwan Brigades, walikutwa na hatia ya kufanya vitendo vya ugaidi, ikiwemo kufyatua risasi kwenye gari la polisi, chanzo cha mahakama kimeiambia AFP.

Hukumu hiyo ambayo imekatiwa rufaa, imelaaniwa na shirika la kutetea haki za binadamu Amnesty International, ambayo limeitaja kama “tusi kwa sheria”, ikitolewa kwa kuvunja utaratibu wa kisheria wa usawa wa haki.

Watu hao wamehukumiwa kuhusiana na matukio ya kati ya Agosti 2013 na Februari 2015, kipindi ambacho kulifanyika mashambulizi mengi, yaliyolenga haswa maafisa wa usalama, kufuatia Jeshi kumuondoa madarakani rais mwenye itikadi kali za kiislamu Mohamed Morsi.

Mahakama iliwapunguzia pia vifungo vya jela watuhumiwa wengine 205 katika kesi hiyo, baadhi wakihukumiwa miaka 10 jela wengine kifungo cha maisha.

Tangu aingie madarakani mwaka wa 2014, mwaka mmoja baada ya kuongoza kuondolewa madarakani kwa Morsi, Rais Abdel Fattah Al-Sisi ameongoza kwa kufanya ukandamizaji mkali dhidi ya wanamgambo wa kiislamu na wapinzani, na kuwatia jela maelfu.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii