Sakaja " Ajiondoe Debeni Kisha Atasemehewa Makosa Yote "

Seneta wa Nairobi Johson Sakaja ameendeleza makombora yake dhidi ya ‘deep state’ kwa kile anachodai ni njama ya kumfungia nje ya uchaguzi mkuu wa Agosti.
Akizungumza katika kanisa la Jesus Winner Ministry mtaani Roysambu katika Kaunti ya Nairobi mnamo Jumapili, Juni 19, Sakaja alidai kuwa viongozi wakubwa wa kisiasa nchini wanamtaka ajiondoe katika kinyang’anyiro cha ugavana wa Nairobi.
Seneta huyo ambaye anachunguzwa kwa madai ya kughushi cheti chake cha shahada alidai kuwa alikuwa ameambiwa ajiondoe katika kinyang’anyiro hicho akihidiwa kuondolewa makosa yote anayodai kusingiziwa.
“Nilipigiwa simu Ijumaa na kuambiwa nijiondoe katika kinyang’anyiro kisha nitakuwa huru. Mnataka nijiondoe uwanjani au niendelee kupambana?” Sakaja aliuliza waumini.
Sakaja aliendelea kwa kupuuza madai kuwa shahada yake kutoka chuo kikuu cha Team nchini Uganda ni gushi na kuwahakikishia waumini kuwa atakuwa debeni Agosti 9.
Kwa mujibu wa seneta huyo, hakuna kiwango cha vitisho au kukamatwa amabko kutamfanya awasaliti wakaazi wa Nairobi anaolenga kuwahudumia kama gavana wao.
“Sisumbuliwi na vitisho vyao vya kunitia mbaroni. Ninaskia wanapanga kunikamata Jumatatu lakini hawatatoboa kwa sababu karatasi zangu ni halali. Hawana kesi dhidi yangu. Tutasimama imara na kuwahudumia watu wa Nairobi,” Sakaja alisema.
Mnamo Jumamosi, Juni 18, Tume ya Huduma kwa Polisi ilithibitisha kuwa ilikuwa imeanzisha uchunguzi kubaini uhalali wa vyeti vya Sakaja na mwenzake wa Machakos Wavinya Ndeti.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii