Tanzania ina upungufu wa vituo vya polisi 470

Serikali imewaomba wabunge, wananchi na wadau kushirikiana katika ujenzi wa vituo vya polisi kwa kuwa ina uhitaji wa vituo vya polisi daraja B, 470

Wito huo umetolewa leo, Aprili 5, 2022 na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusuf Masauni wakati akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Mchinga Salma Kikwete aliyehoji ni lini Serikali itajenga vituo vya polisi katika Kata mbili zilizopo jimboni kwake

Akijibu swali hilo Waziri Masaume amesema kuwa mahitaji ya vituo vya polisi nchini ni makubwa kuliko uwezo wa Serikali kwa kuwa vituo vinavyohitajika ni 563 lakini vilivyopo ni 93 tu kwa nchi nzima.

"Tuna upungufu mkubwa wa vituo vya Polisi, kwa mfano vituo vya Polisi daraja B tunavyo 93 lakini mahitaji ni kuwa na vituo 563, niwaombe wabunge kuiga mfano wa wabunge wengine akiwemo Angelina Mabula ambaye amewashirikisha wananchi kujenga," amesema Masauni.

Katika hatua nyingine majibu ya Waziri kuhusu idadi ya magari ya Polisi 78 ambayo yanatarajiwa kununuliwa, yamezusha maswali bungeni kila mbunge akitaka apewe nafasi ya upendeleo.

Hata hivyo Waziri amesema licha ya mahitaji kuwa makubwa, lakini Serikali itapeleka katika maeneo yenye mahitaji zaidi ya mengine.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii