MOROGORO
Jumla ya Ekari 614 za mashamba ya dawa za kulevya aina ya bangi,
kilogramu 3,741.9 za bangi kavu na kilogramu 1,706 za mbegu za bangi
zimeteketezwa kwenye Hifadhi za Taifa za Mikumi na Nyerere, mkoani Morogoro
Hatua hiyo ni matokeo ya operesheni iliyofanyika
kwa siku tisa mkoani Morogoro kwa ushirikiano kati ya Mamlaka ya Kudhibiti na
Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Hifadhi za
Taifa (Tanapa).
Kwa mujibu wa taarifa kwa umma ambayo imetolewa
leo Julai 16, 2025 na DCEA imesema operesheni hiyo iliyowahusisha pia wananchi,
imewezesha kuvunjwa kwa kambi 72 za wakulima wa bangi na kukamatwa kwa
watuhumiwa tisa wanaohusishwa na zao hilo haramu.
Aidha Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na
Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo amesema kuwa operesheni hiyo ni
sehemu ya mapambano endelevu dhidi ya dawa za kulevya nchini, hususan katika
maeneo yanayozunguka hifadhi za taifa.