Polisi nchini Sierra Leone wamesema wanaendelea na msako dhidi ya watu ambao serikali inasema walihusika na shambulio ambalo lilipangwa katika mji mkuu wa Freetown.
Watu wenye silaha walitekeleza uvamizi dhidi ya ghala la kuhifadhi silaha na magereza kadhaa mjini Freetown siku ya Jumapili, ambapo pia waliwatorosha wafungwa 2,000 gerezani.
Mamlaka inatoa zawadi ya $2,000 (£1,580) kwa yeyote aliye na taarifa kuhusu wahalifu ambao bado hawajulikani walipo, pamoja na $1,000 kwa atakayetoa taarifa kuhusu uwepo wa wafungwa waliotoroka.
Haya yanajiri wakati huu amri ya kutotoka nje usiku kote nchini Sierra Leone ikwia bado inaendelea kutumika baada ya marsharti makali ya awali kulegezwa.
Rais Julius Maada Bio aliwahakikishia raia wa nchi yake kuwa hali ya utulivu imerejeshwa licha ya kilichotokea.
Mkuu wa nchi pia alitaja kilichotokea kama shambulio dhidi ya demokrasia lakini hakuwataja watu waliohusika wala kuzungumzia jaribio hilo la mapinduzi.
Rais Bio alichaguliwa kwa muhula mwengine mwezi Juni lakini mwezi Agosti, baadhi ya maofisa wa jeshi walikamatwa kwa tuhuma za kupanga mapinduzi dhidi yake.