Feisal apitishwa usajili wa Simba SC 2023/24

MAGWIJI wa Simba SC wamesema kama Feisal Salum ‘Fei Toto’ atamaliza kesi yake na Young Africans ni mtu sahihi pale Msimbazi msimu ujao; kwani ana nafasi ya kumtoa mtu katika kikosi cha kwanza cha klabu hiyo na akacheza.

Fei Toto yupo kwenye mvutano na mabosi wake juu ya mkataba, ambapo anataka uvunjwe ili aangalie maisha klabu nyingine kutokana na kile anachodai kuwa ni maslahi duni na pia hana furaha ndani ya Young Africans. Klabu hiyo imemshtaki kwenye mamlaka za soka na kuna shauri linaendelea.

Emmanuel Gabriel ‘Batgol’, Henry Joseph na Joseph Kaniki ‘Golota’ waliong’ara Simba SC kwa nyakati tofauti wamesema pamoja na mambo mengine bado umri wake unamruhusu kung’ara lakini Simba SC wasubiri suala la Fei na mabosi wake litamalizika punde.

Batgol aliyejijengea heshima kwa kuinyanyasa Young Africans katika mechi za watani amesema: “Simba SC wakimsajili Fei watakuwa na bahati na wamelamba dume. Pia atawachangamsha Simba SC na ataleta ushindani ndani ya timu, ana nafasi ya kum- toa mtu akacheza.

“Kikubwa amalizane na Young Africans vizuri ili anakoenda awe huru. Namwamini kuwa ni miongoni mwa wachezaji ambaye anaweza kufanya mabadiliko makubwa kwenye timu.”

Naye Kaniki amesema: “Kwanza Fei umri wake ni mdogo na ana kipaji. Kama watabahatika kumsajili basi litakuwa jambo jema na Fei ana uwezo wa kucheza kwa kocha na timu yoyote, ni suala la mfumo tu.

“Fei yupo kwenye kiwango kizuri na kinapanda. Hizi zingine ni changamoto ambazo wengi wamewahi kuzipitia na maisha yako hivyo.


Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii