Serikali ya Somalia inarudisha fedha ilizozikamata kutoka ndege ya UAE

Serikali ya Somalia imetoa dola milioni 9.6 ilizozikamata kutoka kwenye ndege ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) mjini Mogadishu miaka mine iliyopita hatua inayolenga kurekebisha uhusiano ambao umekuwa sio mzuri tangu wakati huo.

“Pesa zimetolewa na ziko njiani kuelekea Imarati” naibu waziri wa habari wa Somalia Abdirahman Yusuf Al-Adala alisema.

Vyanzo vingine vya kuaminika vya serikali vilisema Waziri Mkuu wa Somalia Mohamed Hussein Roble akiongoza ujumbe alisafiri kwenda Dubai siku ya Jumatano kuwasilisha pesa hizo ana kwa ana.

Pesa hizo zilirejeshwa siku tatu baada ya wabunge wa Somalia kumchagua Rais mpya Hassan Sheikh Mohamud kuchukua nafasi ya mpinzani wa kisiasa wa Roble, Mohammed Abdullahi Mohamed.

Rais mpya wa Somalia ameapishwa lakini bado hajachukua udhibiti wa serikali na inaonekana Roble alichukua hatua hiyo mwenyewe bila ushawishi wowote.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii