Kesi za maambukizi ya Marburg zashuka Rwanda

Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa cha Afrika, CDC, pamoja na wizara ya Afya ya Rwanda, Alhamisi wamesema kuwa kesi za maambukizi ya ugonjwa wa Marburg nchini humo zimeshuka.

Hilo ni kufuatia utoaji wa chanjo kwa watu walioko hatarini zaidi kama wahudumu wa afya, lakini kesi za mpox zinaendelea kuenea kwenye mataifa mengine ya Afrika. Mwanzoni mwa mwezi huu, Rwanda ilianza kutoa chanjo dhidi ya virusi vya Marburg ili kudhibiti ugonjwa huo unaofanana na Ebola.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, waziri wa afya Sabin Nsanzimana, amesema kuwa viwango vya maambukizi vimeshuka kwa zaidi ya asilimia 50 kulinganishwa na wiki za kwanza mbili baada ya kuanza utoaji wa chanjo. Ameongeza kusema kuwa kuna siku ambazo zimekuwa bila maambukizi mapya wala vifo.

Waziri huyo amesema kuwa takwimu za karibuni zaidi zimeonyesha kesi 62 za maambukizi na vifo 15,wakati watu 38 wakipona huku wengine 9 wakiendelea kupokea matibabu. Idadi ya mataifa ya kiafrika yanayoshuhudia maambukizi hayo iliongezeka kutoka 6 hapo Aprili hadi 18 mwezi huu.

Afrika imeshuhudia takriban maambukizi 42,000 ya mpox mwaka huu, vikiwemo vifo 1,100, kulingana na kituo cha CDC. Kaseya amesema kuwa licha ya ahadi ya msaada wa dola milioni 800 kutolewa kwa CDC, ili kupambana na mpox, utekelezaji wa ahadi hizo unajikokota.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii