Mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya wanakutana leo Jumatatu kujadili migogoro inayoendelea nchini Ukraine na Mashariki ya Kati.
Hata hivyo mkutano huo huenda ukagubikwa na suala la hatua ya kihistoria iliyochukuliwa jana na rais wa Marekani Joe Biden ya kutogombea muhula wa pili madarakani.
Mkutano huo unafanyika katika kiwingu cha wasiwasi kote barani Ulaya kuhusu uwezekano wa Donald Trump kurudi tena madarakani nchini Marekani.
Mawaziri hao wanatarajiwa kujadili kuhusu msaada wa Umoja wa Ulaya kwa Ukraine pamoja na uharibifu uliofanywa katika miundo mbinu yake ya nishati, ambayo imekuwa ikishambuliwa na Urusi. Waziri wa mambo ya kigeni wa Ukraine Dmytro Kuleba pia anatarajiwa kujiunga na mkutano huo kwa njia ya video.
Mazungumzo ya Brussels pia yanatarajiwa kujadili hali ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza kufuatia vita vya Israel na Hamas,pamoja na mivutano inayoongezeka katika eneo la mpaka kati ya Israel na Lebanon.