Putin afanya ziara yake ya kwanza Korea Kaskazini baada ya miaka 24

Rais wa Russia Vladimir Putin anatarajiwa kuwasili mjini Pyongyang leo Jumanne katika ziara nadra ambayo inaweza kupelekea kusainiwa “mkataba wa ushirikiano wa kimkakati,” kulingana na maafisa wa Kremlin.

Ikielezewa kama “ziara ya kiserikali ya kirafiki,” ziara hiyo itakuwa ya kwanza kwa Putin kwenda Korea Kaskazini katika kipindi cha miaka 24, huku akitarajia kupata uungwaji mkono katika mashambulizi yake ya kijeshi nchini Ukraine.

Maafisa wa Marekani na Korea Kusini wameishtumu Pyongyang kwa kuipatia Russia zana za kivita, makombora na vifaa vingine vya kijeshi, kama malipo ya kuipa Korea Kaskazini teknolojia muhimu na msaada.

Zote Pyongyang na Moscow zilikanusha tuhuma hizo kuhusu msaada wa silaha za Korea Kaskazini kwa Russia. Maafisa wa serikali ya Ukraine waliripoti kuhusu ndege zisizokuwa na rubani zilizotengenezwa na Korea Kaskazini, zilizogunduliwa kwenye uwanja wa mapigano.

Putin na Kim Jong Un wanatarajiwa kusaini makubaliano mapya ya ushirikiano ambayo yatajumuisha masuala ya usalama, kulingana na mshauri wa sera ya kigeni ya Russia Yuri Ushakov.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii