Zaidi ya watu 100 wameuawa kufuatia mapigano ya kikabila katika jimbo la Dafur Magharibi nchini Sudan.

Mapigano kati ya Waarabu na wapiganaji wa Kiafrika kutoka jamii ya Masalit inayoungwa mkono na waasi wa zamani yamekuwa yakiendelea kwa siku kadhaa sasa. Mapigano katika eneo la Kreinik yamesababisha maelfu ya watu kutoroka makwao, wengine wakivuka mpaka na kuingia nchi jirani ya Chad, Umoja wa Mataifa unasema.

Mmoja wa manusura wa ghasia hizo anasema wanaume waliyojihami walishambulia vijiji vyao magharibi mwa Kreinik, na kuanza kupiga risasi kabla ya kuchoma moto nyumba zao. Pia waliweka vizuizi katika barabara kuu kuwazuia watu kutoroka. Waliojeruhiwa hawana njia ya kupata matibabu ya dharura.Mapigano mapya ya kikabila yalianza Jumapili kati ya jamii hizo mbili, karibu watu 55 wameuawa. Miili zaidi ilipatikana msituni na kuongeza idadi ya vifo hadi zaidi ya 100. Makumi ya wengine hawajulikani waliko.  Mwezi uliopita, watu 43 waliuawa katika sehemu tofauti ya Darfur Magharibi.

Mapigano ya kikabila pia yameripotiwa kusini mwa eneo hilo lenye machafuko. Serikali imetuma kikosi cha pamoja cha vitengo vya kijeshi, jeshi na polisi huko Darfur Magharibi na Kusini ili kujaribu kuzuia ghasia.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii