Israel yaua watoto watatu wa kiongozi mkuu wa Hamas

Israel Jumatano iliwaua watoto watatu wa kiongozi mkuu wa Hamas Ismail Haniyeh katika shambulio la anga huko Gaza, ikisema ndugu hao walikuwa wanachama wa tawi la kijeshi la Hamas.

Wajuku wanne wa Haniyeh waliuawa pia katika shambulio hilo, wakati Hazem, Ameer na Mohammed Haniyeh walikuwa ndani ya gari moja na watoto wao karibu na kambi ya wakimbizi ya Shati mjini Gaza. Ismail Haniyeh ni mzawa wa Shati. Haniyeh ambaye anaishi uhamishoni nchini Qatar, alipata taarifa hiyo akiwatembelea Wapalestina waliojeruhiwa ambao walipelekwa kwenye hospitali ya mjini Doha.

Amethibitisha vifo hivyo katika mahojiano na kituo cha matangazo cha Al Jazeera, akisema watoto wake “waliuawa kama mashuja kwenye barabara wakijielekeza kukomboa Jerusalem na Mskiti wa Al-Aqsa.”

“Adui muhalifu anaongozwa na roho ya kulipiza kisasi na mauaji na hathamini vigezo au sheria zozote,” Haniyeh alisema.

Watoto wake ni miongoni mwa maafisa wakuu kuuawa katika vita vya miezi sita kati ya Israel na Hamas huko Gaza.

Jeshi la Israel limewataja ndugu hao watatu, mmoja kama kamanda na wawili kama maafisa wa kijeshi.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii