Jeshi lasitisha shughuli zote za kisiasa

Utawala wa Jeshi Nchini Mali unaoongozwa na Kanali Assimi Goita umesitisha shughuli zote za vyama vya siasa hadi pale itakapotolewa amri nyingine, ukisema hatua hiyo inalenga kudumisha usalama wa umma.

Amri hiyo, imetolewa baada ya zaidi ya vyama 80 vya siasa na makundi ya kiraia kutoa taarifa ya pamoja Aprili 1, 2024, wakiomba uchaguzi wa rais ufanyike haraka iwezekanavyo na kumalizika kwa utawala wa kijeshi.

Taifa hilo la Afrika magharibi limeongozwa na wanajeshi tangu mapinduzi ya mfululizo mwaka 2020 na 2021, huku hali ya usalama pamoja na mzozo wa kisiasa na kibinadamu ikizidi kuwa mbaya.

Juni 2022, utawala wa kijeshi ulisema uchaguzi wa rais ungefanyika mwezi Februari na utawala kukabidhiwa kwa raia Machi 26, 2024 lakini uliahirishwa na haikutangazwa tarehe nyingine.

Msemaji wa serikali, Kanali Abdoulaye Maiga amefafanua kusimamishwa kwa shughuli za vyama akisema inatokana na majadiliano yaliyokwama wakati wa jitihada za mjadala wa kitaifa mwaka huu.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii