Mwanafunzi awashambulia wanafunzi wenzake kwa bunduki Shuleni Finland

Mwanafunzi mwenye umri wa miaka 12 amefariki na wengine wawili wamejeruhiwa baada ya mwanafunzi mwenzao kuwashambulia kwa bunduki ndani ya shule kusini mwa Finland Jumanne.

Shambulizi hilo limetokea katika mji wa Vantaa wakati masomo yakiendelea.

Mshukiwa huyo aliyeshambulia kwa bunduki, ametambuliwa kuwa ni mwanafunzi mwenye umri wa miaka 12, aliyekimbia kwa miguu na baadae kukamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi.

Taarifa ya hali ya wanafunzi hao wawili ambao walijeruhiwa haijatolewa.

Waziri Mkuu Petteri Orpo alisema “ameshtushwa sana” katika ujumbe aliobandika kwenye mtandao wa kijamii wa X, uliokuwa unajulikana kama Twitter.

Shambulizi la Jumanne ni tukio la karibuni katika shule ya Finland kuwahi kutokea kwa muongo mmoja na nusu.

Mwaka 2007, Pekka-Eric Auvinen mwenye umri wa miaka 18 aliwashambulia kwa bunduki watu tisa, wakiwemo wanafunzi wenzake sita, katika Shule ya Sekondari ya Jokela iliyoko karibu na Helsinki kabla ya kujiua yeye mwenyewe kwa kujipiga risasi.

Watu kumi waliuawa katika kipindi cha chini ya mwaka mmoja baadaye wakati Matti Sarri mwenye umri wa miaka 22 alipoishambulia shule ya ufundi katika mji wa magharibi Kauhajoki kabla ya kujiua.

Finland ina zaidi ya silaha milioni 1.5 zenye leseni na kiasi cha wamiliki wa bunduki wenye leseni 430,000 katika taifa lenye watu milioni 5.6 ambapo uwindaji na ulengaji shabaha ni desturi.

Wabunge waliweka udhibiti wa sheria ya bunduki nchini humo baada ya mashambulizi ya kinyama ya mwaka 2007 na 2008, ikiwemo kuongeza umri wa kumiliki bunduki.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii