Zaidi ya watoto 130 waliokuwa wametekwa nyara Nigeria waokolewa

Zaidi ya watoto wa shule 130 waliotekwa nyara na watu wenye silaha kaskazini magharibi mwa Nigeria mapema mwezi huu waliachiliwa Jumapili bila kujeruhiwa, maafisa na jeshi walisema.

Utekaji nyara huo wa watu wengi huko Kuriga, katika jimbo la Kaduna tarehe 7 Machi, ilikuwa moja ya mashambulizi makubwa kwenye shule kwa miaka kadhaa na kusababisha malalamiko ya nchi nzima juu ya ukosefu wa usalama.

Jeshi lilisema kuwa mateka hao waliachiliwa mapema wakati wa operesheni ya ukoaji lakini halikutoa maelezo zaidi.

Msemaji wa jeshi Jenerali Edward Buba alisambaza picha za watoto hao wakiwa wamevalia zare zenye vumbi ndani ya mabasi.

“Mateka waliookolewa ambao ni jumla ya 137 ni pamoja na wanawake 76 na wanaume 61. Waliokolewa katika jimbo la Zamfara na watafikishwa na kukabidhiwa kwa serikali ya jimbo la Kaduna kwa hatua zaidi,” alisema.

Waalimu na wakazi awali walisema takriban wanafunzi 280 wenye umri wa kati ya miaka minane na 15 walitekwa nyara wakati wahalifu wenye silaha, wanaojulikana kama majambazi nchini Nigeria, walishambulia shule wakiwa kwenye pikipiki.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii